UZINDUZI WA JENIPHER MALL- SERIKALI YAHIMIZWA KUWAWEZESHA KINA MAMA KIUCHUMI PASIPO MASHARTI MAGUMU YA MIKOPO




Na Carlos Claudio, Dodoma.📍


Serikali imetakiwa kuweka mikakati madhubuti ya kuwawezesha kina mama, hususan wale waliopo majumbani wenye juhudi za kufanya biashara lakini wanakwamishwa na ukosefu wa mitaji pamoja na masharti magumu ya mikopo kutoka taasisi za kifedha.


Wito huo umetolewa leo Januari 25, 2026 jijini Dodoma na Mkurugenzi Mtendaji (CEO) wa Jenipher Mall, Jenipher Samuel, wakati wa uzinduzi wa duka hilo jipya la biashara linalojihusisha na uuzaji wa bidhaa mbalimbali za majumbani ikiwemo vyombo vya ndani, mapambo ya ndani na mahitaji mengine ya kifamilia.


Jenipher amesema kuwa wanawake wengi wana ndoto na nguvu ya kufanya biashara, lakini hukwama wanapohitaji mtaji kwa sababu benki na taasisi nyingi za fedha zinahitaji dhamana zisizohamishika kama nyumba au viwanja ambavyo wengi hawana.


“Serikali itusaidie kupata mifumo rafiki ya mikopo pasipo masharti magumu ili kuepusha kuzikwa kwa ndoto za wajasiriamali wenye uwezo na juhudi,” amesema Jenipher.


WANAWAKE WAKIFANIKIWA HAWAPUUZI FAMILIA


Akizungumzia mitazamo hasi iliyopo kwa baadhi ya wanaume, Jenipher amesema kuwa kuna imani potofu kuwa mwanamke anapofanikiwa huweza kuwadharau waume zao au kupuuza majukumu ya kifamilia, hali ambayo amesema si ya kweli.


“Zipo familia nyingi ambazo wanawake wamefanikiwa lakini bado ni wake bora na mama wazuri. Mafanikio ya mwanamke hayamaanishi kuvunjika kwa familia,” amesema.


Ametoa wito kwa wanaume kuwa na imani kubwa kwa wanawake zao wanapoonesha juhudi za kupiga hatua kimaisha, akisema kuwa hilo ni nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa familia na taifa kwa ujumla.


MUME WANGU NI NGUZO YA MAFANIKIO YANGU


Jenipher hakusita kutambua mchango mkubwa wa mume wake katika safari yake ya mafanikio, akisema kuwa imani, msaada wa kifedha na moyo wa kumuunga mkono vimekuwa msingi mkubwa wa hatua alizofikia leo.


“Kama nisingepata imani yake na ruhusa ya kutoka nje kuonesha uwezo wangu, nadhani kile mnachokiona leo kisingekuwepo,” amesema.


SAFARI YA JENIPHER MALL KUTOKA MILIONI TATU HADI KUWA MALL


Akielezea safari ya biashara yake, Jenipher amesema alianza na mtaji wa shilingi milioni tatu pekee, ambapo alichukua mzigo wa biashara wenye thamani ya shilingi milioni mbili laki tisa sabini na tano kutoka kwa mfanyabiashara aliyemtaja kwa jina la Sekela wa Ramsek.


Kwa msaada na ushauri alioupata, alianza kuuza bidhaa zake hatua kwa hatua kuanzia maeneo ya vichochoroni hadi kufikia hatua ya nne ya ukuaji wa biashara ambayo sasa ni Jenipher Mall.


BIDHAA BORA KWA BEI RAFIKI KWA KILA MTANZANIA


Jenipher amesema kuwa mall hiyo imejikita katika kutoa bidhaa bora kwa bei nafuu ili hata Mtanzania wa kipato cha chini aweze kumudu.


“Jenipher Mall ina kila aina ya bidhaa za majumbani, zenye ubora wa juu lakini kwa bei ya chini na rafiki kwa kila mmoja,” amesema.


Ameongeza kuwa mall hiyo imeleta bidhaa ambazo awali hazikupatikana jijini Dodoma, hali iliyowalazimu wananchi wengi kuagiza kutoka Dar es Salaam.


MKAKATI WA KUFIKIA TANZANIA YOTE NA MNADA WA BEI FUPI


Jenipher amesema kuwa matarajio ya Jenipher Mall ni kufika mikoa yote ya Tanzania kwa kufungua matawi mbalimbali, sambamba na kuanzisha mkakati wa mnada wa bei fupi unaotembea mikoa yote.


Amesema mnada huo utawarahisishia wateja waliopo mikoani ambao hawana imani ya kuagiza bidhaa kwa njia ya mtandaoni.


UJUMBE KWA WAJASIRIAMALI WADOGO


Akihitimisha hotuba yake, Jenipher amewahimiza wajasiriamali wadogo kuwekeza katika juhudi, kuwa na nidhamu ya fedha, uaminifu na bidii, akisisitiza kuwa kwa misingi hiyo, hakuna kisichowezekana.

“Ukijitoa, ukawa mwaminifu na mwenye nidhamu ya fedha, mafanikio yanawezekana,” amesema.













🚨Full Video Inapatikana Katika YOUTUBE Channel Yetu Ya WASHINDI MEDIA

Previous Post Next Post