Nairobi, Kenya.📍
Shirika la Bima la Taifa la Tanzania (NIC) limepata tuzo ya Superbrand kwa mara ya pili mfululizo, hatua inayothibitisha sifa yake kama moja ya watoa huduma za bima wanaoaminika zaidi katika ukanda huu na kuonyesha kuimarika kwa mchango wake katika sekta ya huduma za kifedha Afrika Mashariki.
Tuzo hiyo ilitangazwa rasmi katika Hafla ya Superbrands Tribute iliyofanyika jijini Nairobi, mkutano wa ngazi ya juu uliowakutanisha zaidi ya viongozi wakuu 200 kutoka mataifa mbalimbali ya ukanda huu. NIC ilichaguliwa chini ya mpango wa Superbrands Volume 9, unaopima chapa kwa kuzingatia vigezo vya uaminifu, ubora wa huduma, sifa njema, na uongozi wa soko.
Tuzo hiyo ilipokelewa na Bw. Karimu Meshack, Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano aliyeiwakilisha NIC katika hafla hiyo, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa NIC, Bw. Kaimu Abdi Mkeyenge.
Wachambuzi wa sekta ya bima wanaeleza kuwa kupokea tuzo ya Superbrand kwa mara ya pili mfululizo ni ishara ya uthabiti wa Shirika katika sekta ambayo uaminifu na uhakika wa huduma ni nguzo muhimu.
Mafanikio haya yanaakisi juhudi za NIC katika kuimarisha utawala bora, kuboresha mifumo ya utoaji huduma, na kuongeza ushirikiano na wateja katika soko la bima lenye ushindani na mabadiliko ya haraka.
NIC ilianzishwa mwaka 1963 ikiwa ni mtoa huduma za bima wa taifa, ikitoa huduma za Bima za Maisha na Bima za Mali na Ajali kwa watu binafsi, taasisi za umma, na sekta binafsi.
Katika miaka ya hivi karibuni, Shirika limeongeza kasi ya mageuzi kwa kupanua upatikanaji wa huduma za kidijitali kupitia majukwaa kama NIC Kiganjani, Tovuti ya Shirika, na Chatbot, kuboresha mifumo ya ulipaji wa madai, na kuoanisha shughuli zake na viwango bora vya kimataifa.
Mafanikio haya yanakuja wakati NIC ikiendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa Shirika 2026–2030, unaolenga kukuza ukuaji endelevu, kuboresha huduma kwa wateja, kuharakisha mageuzi ya kidijitali, na kuimarisha mifumo ya utawala. Nguzo hizi za kimkakati zinaendana pia na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayosisitiza umuhimu wa taasisi imara na zinazostahimili mabadiliko katika kukuza maendeleo ya uchumi wa muda mrefu.
Katika mazingira ambapo ongezeko la matumizi ya bima linaendelea kuwa kichocheo muhimu cha utulivu wa uchumi katika masoko yanayochipukia, kuendelea kutambuliwa kwa NIC kunadhihirisha mchango wa taasisi za serikali zinazoaminika katika kukuza ujumuishaji wa kifedha, ulinzi dhidi wa majanga, na kuimarisha imani ya wawekezaji.
NIC itaendelea kuzingatia na kuimarisha uaminifu wa wateja, kupanua matumizi ya majukwaa ya kidijitali, na kuendeleza nafasi ya Shirika kama mshirika wa kuaminika kwa kaya, biashara, na Serikali, ndani ya Tanzania na katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki.
🚨Subscribe YOUTUBE Channel Yetu Ya WASHINDI MEDIA.




