NACTVET YAHUISHA MIONGOZO MIPYA KUBORESHA AJIRA KWA VIJANA



Na Carlos Claudio, Dodoma.📍


Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limefanya maboresho mapya ya miongozo yake ya elimu ili kuhakikisha vijana wanaomaliza masomo katika vyuo vya ufundi nchini hawakumbwi na changamoto ya ukosefu wa ajira.



Akizungumza leo Novemba 18, 2025 jijini Dodoma katika warsha maalum ya kutoa taarifa kuhusu miongozo hiyo, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa NACTVET, Bernadetha Ndunguru, alisema kuwa maboresho hayo yamefanyika kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya soko la ajira na dira ya nchi katika kuendeleza nguvu kazi yenye ujuzi na ubunifu.


Ndunguru alibainisha kuwa mabadiliko hayo ni sehemu ya jitihada endelevu za serikali kuhakikisha elimu ya ufundi inaendana na mahitaji ya viwanda, sekta binafsi pamoja na mabadiliko ya teknolojia duniani.



Kwa upande wake, Mkurugenzi wa NACTVET, Dkt. Mwajuma Lingwanda, alisema kuwa maboresho ya miongozo hiyo yataleta mageuzi katika viwango vya ubora wa elimu ya ufundi, ikijumuisha kuboresha mitaala, kuongeza mbinu za ufundishaji na kuimarisha uhusiano kati ya vyuo na waajiri.


“Athari ya moja kwa moja ya maboresho haya ni kukuza soko la ajira kwa wanafunzi, kuwaongezea uwezo wa ushindani, na kuhakikisha kwamba wahitimu wanakuwa tayari kuingia kwenye dunia ya kazi bila changamoto,” alisema Dkt. Lingwanda.


Aidha, baraza hilo limeahidi kuendelea kusimamia ubora wa elimu katika vyuo vya ufundi nchini pamoja na kupanua wigo wa udahili ili kutoa fursa zaidi kwa vijana kupata elimu na ujuzi utakaowawezesha kujitegemea.


Warsha hiyo imetoa taswira mpya ya mwelekeo wa elimu ya ufundi nchini, ikionyesha dhamira ya dhati ya NACTVET katika kuleta mageuzi chanya yatakayochochea maendeleo endelevu ya kiuchumi kupitia nguvu kazi iliyobobea katika ujuzi.






🚨Subscribe YouTUBE Channel yetu ya WASHINDI MEDIA.

Previous Post Next Post