VIONGOZI WA DINI NA SERIKALI WAHIMIZWA HAKI, UMOJA NA MAOMBI KWA MUSTAKABALI WA TAIFA.

 


Na Carlos Claudio, Dodoma.📍


Viongozi wa dini na serikali nchini wametakiwa kusimamia haki, usawa na kuendeleza maombi kwa ajili ya taifa ili kuhakikisha Tanzania inaendelea kubaki katika amani, umoja na baraka za Mungu.


Wito huo umetolewa leo Desemba 27, 2025 jijini Dodoma na Askofu Dkt. Mussa Mlawi, Raisi wa Tanzania Pastors Association (TPA), wakati wa ibada maalum ya kuliombea taifa la Tanzania pamoja na kuwatunuku wahitimu wa mahafali ya 14 ya Chuo cha Africa Bible College International Tanzania (ABCI-T).


Askofu Dkt. Mlawi alisema licha ya kasoro na uzembe uliowahi kujitokeza hapo nyuma kwa upande wa viongozi wa dini na serikali, bado taifa lina nafasi ya kurejea kwa Mungu kwa toba ya kweli ili liendelee kupokea baraka na ulinzi wake. 


Alisisitiza kuwa baraka za taifa hazitoki kwa wanadamu bali zinatoka kwa Mungu, hivyo ni wajibu wa taifa zima kumtanguliza Mungu katika kila jambo.


“Taifa letu linahitaji kuungana, kuacha matabaka na migawanyiko ya makundi, tuwe na sauti moja, lugha moja na kauli moja ya kulinda amani ya nchi yetu. Mungu akikasirika, kurejesha amani huwa ni jambo gumu,” alisema Askofu Mlawi.


Aliongeza kuwa mivutano ya kauli na misimamo tofauti baina ya makundi mbalimbali haiwezi kulijenga taifa, bali kinachohitajika ni taifa kurejea kwa Mungu, kutubu na viongozi wa dini kujitathmini ni wapi walimkosea Mungu na kurekebisha njia zao.


Katika maombi hayo, viongozi wa dini waliomba Mungu kuliepusha taifa na majaribu yanayoweza kuisukuma nchi kwenye machafuko, huku wakisisitiza kuwa maombi hayo yamewakilisha kuanzia ngazi ya mkoa hadi taifa zima. 


Askofu Mlawi alitoa wito kwa viongozi wote wa kiroho na kidini nchini kuendeleza maombi kama hayo kila mahali ili neema ya Mungu iendelee kutiririka juu ya Tanzania.



Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, alisema anatambua kuwepo kwa changamoto mbalimbali nchini, lakini aliwasihi viongozi wa dini kuendelea kuwa imara katika kuiombea amani ya nchi.

“Serikali ina majukumu yake na dini ina majukumu yake. Nyinyi ni viongozi wetu wa kiroho, endeleeni kutulea kiimani ili tuwe watu wema,” alisema Mhe. Mayanja.


Pia aliwataka Watanzania kuendelea kuwaombea viongozi wa serikali akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili waendelee kuwa na maono mapana ya kuwatumikia wananchi, akisisitiza kuwa Tanzania ni nchi pekee waliyonayo Watanzania.



Naye Makamu wa Raisi wa Tanzania Pastors Association (TPA) ambaye pia ni Raisi na Muasisi wa huduma Barani Africa, Prof. Margareth Kilimali alisema elimu ni jambo la msingi hata kwa watumishi wa Mungu, akibainisha kuwa kwa muda mrefu baadhi ya watumishi walidhani kusoma ni kupoteza muda, ilhali elimu huongeza maarifa na uwezo wa kuwahudumia watu wa makundi yote kwa usawa.

“Hata Neno la Mungu linatuhimiza tusiiache elimu. Elimu isiwe kwa ajili ya kupata vyeti vya kupamba kuta za nyumba, bali iwe ni chombo cha kuwasaidia wachungaji kukutana na mahitaji halisi ya watu wanaowahudumia,” alisema Prof. Kilimali, akiwahimiza wahitimu kuendelea kujifunza hata baada ya kuhitimu.



Kwa upande wake, Mchungaji Neema Philipo Lumambo wa Kanisa la International Church of New Testament Tanzania (ICNT), ambaye pia ni mhitimu wa ngazi ya Diploma, alimshukuru Askofu Dkt. Mussa Mamlawi kwa kuwa mlezi na mkombozi wa wachungaji wengi nchini.

“Wachungaji wengi tulikuwa na changamoto na hatukuona tumaini la kusonga mbele, lakini Askofu Dkt. Mlawi alikuwa na maono ya kutuona tukipiga hatua. Kupitia huduma yake, nimefanikiwa kufungua kanisa langu mwaka jana,” alisema Mchungaji Neema.


Ibada hiyo ilihitimishwa kwa maombi ya pamoja ya kuliweka taifa mikononi mwa Mungu, huku viongozi wakisisitiza kuwa amani, umoja, mshikamano na upendo ni nguzo muhimu zitakazoiwezesha Tanzania kuendelea kuwa kisiwa cha amani na mahali salama pa kuishi.
















🚨Full Video Inapatikana Katika Youtube Channel Yetu Ya WASHINDI MEDIA.

Previous Post Next Post